HOTUBA YA MHE JAJI MKUU WA ZANZIBAR KWENYE MKUTANO MKUU WA ZAJAO 2023
HOTUBA YA JAJI MKUU WA ZANZIBAR MHE. KHAMIS RAMADHAN
ABDALLA KATIKA UFUNGUZI WA MKUTANO MKUU WA ZAJOA WA MWAKA 2023
PAHALA: UKUMBI WA CHUO CHA UTALII MARUHUBI
TAREHE 06 APRILI, 2023.
MHESHIMIWA MWENYEKITI,
WAHESHMIWA MAJAJI WA MAHKAMA KUU MLIOPO,
MHESHMIWA KADHI MKUU WA ZANZIBAR,
MHESHMIWA NAIBU KADHI MKUU WA ZANZIBAR,
MHESHMIWA KADHI WA RUFAA PEMBA,
MHESHMIWA MTENDAJI MKUU WA MAHKAMA,
MHESHIWA MRAJIS WA MAHKAMA YA KADHI,
NAIBU WARAJIS WOTE MLIOPO,
WAHESHIMIWA WAJUMBE WOTE,
WAALIKWA NA WAFANYAKAZI WOTE WA MAHKAMA MLIOPO,
WAANDISHI WA HABARI,
MABIBI NA MABWANA,
ASALAM ALAYKUM ,
Ndugu
Mwenyekiti,
Awali
ya yote napenda kuchukua fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema
na utukufu kwa kutuvusha salama katika mwaka uliopita wa 2022 na kuingia mwaka mpya wa 2023 tukiwa tupo hai kwani baadhi yetu wameshatangulia akhera, Allah awape makaazi
mema peponi Amin. Aidha, namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujaalia afya njema,
salama, amani na utulivu katika nchi yetu na leo tumeweza kukutana hapa kwa
ajili ya mkutano huu adhimu wa mwaka.
Ndugu
Mwenyekiti na wajumbe,
Napenda
kuchukua fursa hii, kuushukuru Uongozi wa ZAJOA kwa ujumla kwa kunialika tena kwa mara nyengine kuwa, Mgeni rasmi katika ufunguzi
wa mkutano huu wa mwaka na pia kuhudhuria mimi mwenyewe nikiwa ni mlezi wa
ZAJOA na mjumbe wa mkutano huu. Hii ni fursa adhimu kwangu kwani huniwezesha
kujumuika na waheshimiwa Majaji, Mahakimu na Makadhi na kupata wasaa wa
kufahamu mafanikio na changamoto za ZAJOA na Mahkama kwa ujumla kwa mwaka uliopita pamoja na kufahamu malengo na mikakati
kwa mwaka ujao ili kuboresha na kuimarisha utendaji kazi na utoaji haki nchini
na hivyo, kuleta maendeleo ya Taifa kwa ujumla.
Ndugu
Mwenyekiti,
Napenda
kuipongeza ZAJOA kwa kuweza
kuiwakilisha vizuri Mahkama Zanzibar na kushiriki kikamilifu katika mkutano wa EAMJA uliofanyika Kigali Rwanda mwaka jana
ingawa mimi mwenyewe sikuweza kushiriki kutokana na majukumu mengine
yaliyojitokeza lakini taarifa nilizopewa ni kuwa, mambo yamekwenda vizuri.
Sambamba na hilo nawashukuru kwa dhati kabisa waheshimiwa Majaji, Mahakimu na
Makadhi wote kwa kushiriki kikamilifu na kufanikisha maadhimisho ya siku ya
sheria “LAW DAY“ ya mwaka huu.
Nyote
mlikua ni mashahidi kwamba, sherehe zetu za siku ya sheria za mwaka huu zilikua
na mambo mengi mapya na ya ubunifu mkubwa kama vile mbio za marathon, uzinduzi wa ripoti
ya mwaka ya utendaji kazi wa Mahkama, utoaji wa zawadi kwa vinara wa utoaji wa
haki n.k, tujipongeze sote kwani sherehe zetu za siku ya sheria za mwaka huu
zilifana sana kinyume na matarajio yetu.
Ndugu
Mwenyekiti,
ZAJOA imeniarifu rasmi kwamba, mkutano wa Baraza kuu la Majaji na Mahakimu wa Afrika Mashariki (EAMJA COUNCIL MEETING) utafanyika hapa Zanzibar mnamo tarehe 23,
juni 2023. Napenda kuwahakikishia kwamba, uongozi wa Mahkama kwa mashirikiano na ZAJOA utafanya kila kinachowezekana kuhakikisha kua, mkutano huo
unafanyika kwa mafanikio makubwa na kuiletea sifa nchi yetu.
Ndugu Mwenyekiti,
Sasa
nizungumzie utendaji kazi wetu wa Mahkama kwa mwaka uliopita. Ripoti ya tathmini ya utendaji kazi wa
Mahkama inaonyesha kwamba, kwa ujumla, kwa
mwaka 2022, Mahkama za Zanzibar zimeweza kumaliza mashauri ya jinai kwa
asilimia 91.7% na kwa kesi za madai, kasi ya umalizikaji wa mashauri ni
asilimia 54.9%. Takwimu hizo zinaonyesha kwamba, hali ya umalizikaji wa mashauri ya jinai ni
nzuri sana na kwa upande wa mashauri ya madai ni nzuri kiasi.
Napenda
kuchukua fursa hii kuwapongeza kwa dhati , Waheshimiwa Majaji, Mahakimu,
Warajis, Makadhi na Watumishi wote wa Mahkama kwa ari na moyo wa utendaji kazi
tuliouonyesha kwa mwaka uliopita wa 2022. Mafanikio haya yasingepatikana kama sote tusingefanya kazi ya ziada.
Aidha
pongezi ziwaendee wadau wetu wakuu ambao ni Afisi ya Mwanasheria Mkuu, Afisi ya
Mkurugenzi wa Mashtaka, Jeshi la Polisi, Mamlaka ya Kupambana na Rushwa na
Uhujumu Uchumi (ZAECA), Mamlaka ya
Kudhibiti na Kupambana na madawa ya Kulevya, Chama cha Mawakili, Asasi za
Kiraia na bila ya kuwasahau watu wenye mashauri (Wadaawa)
Ndugu Mwenyekiti,
Napenda
nieleze kwamba, licha ya juhudi mbali mbali zinazochukuliwa na Serikali yetu ya
Mapinduzi ya Zanzibar katika kuboresha utendaji kazi wa Mahkama, bado
tunakabiliwa na changamoto kadhaa kama vile uhaba wa watumishi uliosababishwa
na watumishi wetu wengi kufikia umri wa kustaafu na wengine kufariki, uchakavu
wa majengo na vitendea kazi n.k. Hata hivyo, niwahakikishie kua, kwa
kushirikiana na Serikali yetu, tunaendelea kuzifanyia kazi changamoto hizo kwa
lengo la kuzipatia ufumbuzi. Kwa mfano, katika kukabiliana na changamoto ya
uhaba wa watumishi, kwa mwaka 2022/2023 serikali imeturuhusu kuajiri Makatibu
muhtasi watano (5) na Maofisa Sheria watatu (3). Aidha, baada ya Serikali
kupitisha muudo wa utawala wa Mahkama, tumepewa kibali cha kuajiri Mkurugenzi
Mipango na Utafiti pamoja na Mkurugenzi Rasilimali watu na Utawala. Mchakato wa
uajiri kwa watumishi wote hao upo kwenye hatua za mwisho na tunataraji hivi
karibuni wataajiriwa. Kuajiriwa kwa watumishi hao kutasaidia sana kuongeza
ufanisi katika shughuli zetu. Halkadhalika, katika mwaka mpya wa fedha wa
23/24, pia tutaendelea na zoezi la uajiri wa wafanyakazi wapya kwa lengo la
kuziba mapengo ya watumishi (replacement) kwenye taasisi yetu.
Ndugu
Mwenyekiti,
Hivi
karibuni uongozi wa Mahkama uliamua kuwa, mfumo wa upandaji vyeo kwenye mhimili
wetu uwe wa uwazi zaidi kwa nafasi husika kutangazwa na waombaji wakiwemo
watumishi wetu wa Mahkama kuomba nafasi hizo na baadae kufanyiwa usaili.
Tumeanzisha mfumo huu kwa nia njema kabisa ya kupata watendaji wenye sifa
stahiki pamoja na kuondoa malalamiko yanayojitokeza kila tunapofanya mchakato
wa upandishaji vyeo. Aidha, mfumo huu ni maarufu sana katika nchi za majirani
zetu. Ombi langu kwenu ni kua, kwa wale watakaobahatika kupanda vyeo, waonyeshe
kwa vitendo kuwa kweli walistahiki kupata nafasi hizo na wakati huo kwa wale
ambao hawatobahatika kupata nafasi hizo, basi wasivunjike wala kukasirika bali
nao wazidishe ari ya kufanya kazi huku wakijuwa kua, kuna fursa nyingi tu za
wao kupanda madaraja muda si mrefu. Naipongeza sana Tume ya Utumishi wa Mahkama
pamoja na Afisi ya Mtendaji Mkuu na ile ya Mrajis wa Mahkama kwa kusimamia kwa
umakini zoezi hilo la ajira.
Ndugu
Mwenyekiti,
Kama
tulivyoeleza wakati wa maadhimisho ya siku ya sheria ya mwaka huu
kua,tumedhamiria kuelekea kwenye Mahkama Mtandao. Hivi sasa tupo kwenye hatua
za mwisho zitakazotuwezesha kuingia kwenye uanzishaji wa mifumo mbali mbali ya
kidijitali itakayorahisisha utendaji wetu wa kazi. Wakati hayo yakiendelea,
natowa wito kwa watumishi wote wa Mahkama kujiendeleza katika fani ya
teknolojia ya habari na matumizi ya Tehama ili wasije wakaachwa nyuma kwenye
mabadiliko hayo ya kidigitali. Halkadhalika, Mahakama kwa kushirikiana na
Serikali itaweka mazingira mazuri kwa ajili ya matumizi ya Tehama kama vile
ujenzi wa majengo bora na ya kisasa ya Mahkama ili kuifanya azma hiyo ya
mahakama mtandao iwe rahisi kutekelezeka.
Ndugu
Mwenyekiti,
Serikali
yetu inaelewa kuwa, mazingira mazuri ya utoaji haki ni lazima yaendane sambamba
na uboreshaji wa maslahi ya watumishi wa sekta ya sheria. Hivyo, kuipitia mkutano
huu napenda kuipongeza serikali yetu kwa kuongeza kwa kiasi kikubwa maslahi ya
watumishi wa Mahkama pamoja na kumaliza kilio cha siku nyingi cha mishahara ya
Mahakimu wa Mahkama za mwanzo. Aidha, Serikali imeridhia ombi letu la kuwalipa
posho la mavazi (outfit allowance) watumishi wote wa Mahkama.
Nimefurahi
sana baada ya Ofisi ya Mtendaji Mkuu wa Mahkama kuniarifu kuwa, zoezi la
kuwalipa posho la mavazi watumishi wote
wa Mahkama limeanza na limeanzia kwa watumishi wa kada za chini kama vile
matarishi, madereva, makarani n.k. Ni matumaini yangu kuwa, hatua hizo zitakuwa
ni chachu ya kuongeza ari ya kufanya kazi kwa watumishi wetu.
Ndugu
Mwenyekiti,
Nimefahamishwa
kwamba, pamoja na mambo mengine, katika mkutano huu kutafanyika uchaguzi mkuu
wa viongozi mbali mbali wa ZAJOA. Natowa wito kwa wajumbe, kuwachaguwa viongozi
wenye sifa ambao watakuwa na uwezo mkubwa wa kutatua changamoto mbali mbali za
ZAJOA ikiwemo ubunifu wa vyanzo mbali mbali vya mapato pamoja na kuiwalisha
vizuri ZAJOA kwenye mikutano ya kimataifa. Halkadhalika, natowa wito kwa
uongozi mpya wa ZAJOA utakaiongia madarakani baada ya uchaguzi kutengeneza
mpango mkakati wa mafunzo kwa wanachama wake. Hii ni kwa sababu, fani ya sheria
imekuwa inakuwa kwa kasi sana, hivyo wanachama wa ZAJOA wakiwemo Majaji,
Mahakimu na Makadhi wanahitaji kupatiwa mafunzo ya mara kwa mara kwa lengo la
kukuza uelewa wao kwenye mambo mbali mbali yanayousu utendaji kazi wao.
Ndugu
Mwenyekiti,
Nimefurahi
sana baada ya kuambiwa kuwa mkutano huo utatanguliwa na uwasilishaji wa mada
inayohusu njia za kudhibiti msongo wa mawazo (stress Management) pamoja
na salamu za Benki ya NMB. Kwanza, nawapongeza na ninawashukuru watayarishaji
wa mada zote zitakazowasilishwa hapa kwa uzalendo wao. Kwa upande wa mada ya
kuondoa msongo wa mawazo, nasema kuwa ni mada muhimu sana kwa watendaji wa
Mahkama hasa kwa vile itaimarisha afya ya akili zetu kutokana na kazi ngumu
tulizonazo. Vile vile kwa upande wa Benki ya NMB nao nawashukuru na ninawaomba
watuunge mkono katika shughuli zetu mbali mbali za kimahkama zitakazofuata.
Ndugu
Mwenyekiti,
Kwa
kumalizia,napenda nitowe wito kwa ZAJOA
kuwa, katika mkutano mkuu wa mwakani wa ZAJOA tutenge siku mbili ambapo siku ya
kwanza iwe ni kwa ajili ya mafunzo na mambo mengine kama vile upimaji wa afya
(medical checkup) n.k na siku ya pili iwe ni kwa ajili ya kufanya mkutano mkuu.
Uongozi wa Mhkama upo tayari kuiwezesha ZAJOA kutatuwa changamoto mbali mbali
inazozikabili kila hali itakaporuhusu. Mwisho kabisa nawaomba wajumbe wote
kutumia mkutano huu kujadili changamoto mbali mbali zinazoikabili Mahkama na
ZAJOA kwa njia za kistaarabu bila ya kumkwaza mtu na kupendekeza ufumbuzi wake.
Nawatakia mkutano mwema na sasa natangaza rasmi kua,
MKUTANO
HUU MKUU WA ZAJOA WA MWAKA 2023 UMEFUNGULIWA RASMI. AHSANTENI KWA KUNISIKILIZA.