Registrar: registrar@judiciaryzanzibar.go.tz | Chief Court Administrator: cca@judiciaryzanzibar.go.tz

THE JUDICIARY OF ZANZIBAR

HUTUBA YA WAZIRI LUKUVI KATIKA UWEKAJI WA JIWE LA MSINGI MAHKAMA YA WILAYA YA MKOA

HOTUBA YA MHE. WILLIAM V. LUKUVI (MB.) WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU (SERA, BUNGE NA URATIBU) KATIKA HAFLA YA UWEKAJI WA JIWE LA MSINGI KATIKA UJENZI WA JENGO JIPYA LA MAHKAMA YA WILAYA YA MICHEWENI

TAREHE 04 JANUARI, 2025

Mheshimiwa Khamis Ramadhani Abdalla, Jaji Mkuu wa Zanzibar;

Mheshimiwa Rashid Hadidi Rashid, Mkuu wa Mikoa wa Kusini Pemba;

Ndugu Yusuph Ali Juma, Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Kusini Pemba;

Waheshimiwa Majaji mliopo mkiongozwa na Mhe. Jaji Salum Hassan Bakar, Jaji Mkazi - Pemba;

Mheshimiwa Othman Ame Chumu, Naibu Kadhi Mkuu;

Mheshimiwa Hamad Omar Bakar, Mkuu wa Wilaya ya Mkoani;

Waheshimiwa Wabunge na Wawakilishi mliopo;

Mheshimiwa Valentina Katema, Mrajis wa Mahkama Kuu;

Waheshimiwa Mahakimu na Makadhi wa ngazi mbali mbali;

Waheshimiwa Viongozi wa Vyama vya Siasa na Serikali;

Waheshimiwa Viongozi wa Dini;

Wakuu wa Vikosi vya Ulinzi na Usalama wa SMT na SMZ mliopo;

Waheshimiwa Mawakili wa Serikali na Mawakili wa Kujitegemea;

Ndugu Watumishi wa Umma na Wanahabari mliopo;

Wageni Waalikwa - Mabibi na Mabwana.

Assalaam Aleiykum

Mheshimiwa Jaji Mkuu, Ndugu Viongozi mliopo na wananchi wote.

Niungane na walionitangulia kumshukuru Mwenyezi Mungu Mtukufu mwingi wa rehma kwa kutujaalia uzima na afya iliyotuwezesha kukutana katika hafla hii muhimu ya uwekaji wa jiwe la msingi katika ujenzi wa jengo jipya la Mahakama ya Wilaya ya Micheweni.


Pili niwaashukuru sana kwa kunialika kuwa Mgeni Rasmi katika hafla hii adhimu. Mwaliko wenu umenipa fursa ya kujumuika na Wananchi wenzangu hususani wa Wilaya ya Mkoani pamoja na wananchi wengine waliofika katika sherehe hii ya uwekaji wa jiwe la msingi la ujenzi wa jengo jipya la Mahkama ya Wilaya ya Mkoani hapa Changaweni. Sambamba na hilo, niwashukuru na kuwapongeza viongozi na wananchi wote mliojitokeza katika sherehe hii ambayo ni sehemu ya Maadhimisho ya Miaka 61 ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar ya mwaka 1964.


Ndugu Viongozi na wananchi wote,

Sote ni mshahidi wa hatua kubwa za maendeleo zinazoendelea kutekelezwa na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kupitia uongozi wa awamu ya nane chini ya Mhe. Daktari Hussein Ali Mwinyi, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi. Mafanikio ya Serikali ya awamu ya nane yanaonekana wazi katika nyanja za siasa na utawala bora, uchumi, huduma za kijamii na namna utamaduni wa watu wa Visiwa vya Zanzibar unavyoenziwa na kuheshimika wakati wote.


Maendeleo katika nyanja hizi yanashuhudiwa vizuri katika maeneo mbalimbali kupitia ujenzi wa miundombinu ya mawasiliano, majengo ya ofisi, majengo ya kutolea huduma za kijamii pamoja na msisitizo uliowekwa kwenye uchumi wa buluu, uvuvi na kilimo cha mwani.  Kwa upande wa ujenzi wa majengo ya Ofisi, mpango ya Serikali ya Zanzibar ni kuhakikisha yanajengwa majengo ya kisasa ya ofisi ili kuimarisha mazingira bora ya kufanyia kazi na kuchochea utoaji wa huduma bora kwa wananchi.


Ndugu Viongozi na wananchi wote,

Tunafahamu kwa miaka mingi Mahakama zetu zimekuwa na changamoto za miundombinu ya majengo. Kwa mfano jengo linalotumika hivi sasa kwa shughuli za Mahakama ya Wilaya halikidhi mahitaji halisi ya Mahakama kwa sasa. Pamoja na ufinyu wa nafasi, jengo hilo pia si rafiki kwa watumiaji wenye mahitaji maalumu. Wananchi wanaofika kufuata huduma muda mwingi wanakosa sehemu maalum ya kupumzikia au kusubiri kuhudumiwa.


Hali hii ndiyo iliyoipelekea Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kuchukua hatua za makusudi kuja na mradi wa ujenzi wa jengo hili la Mahakam ya Wilaya pamoja na majengo mengine ya Mahakama za Mikoa na Wilaya kule Unguja na hapa Pemba.  Hivyo, ujenzi wa jengo hili ni sehemu ya utekelezaji wa Mradi wa ujenzi wa majengo saba ambao ulipangwa kufanyika katika mwaka wa fedha wa 2023/2024. Kwa upande wa Pemba, mradi huu wa Loti Nambari 2 unajumuisha majengo matatu (Mahakama ya Mkoa wa Kaskazini, Mahakama ya Wilaya ya Michweweni na Mahakama ya Wilaya ya Mkoani hapa Changaweni)


Ndugu Viongozi na wananchi wote,

Kwa upande wa jengo hili, ujenzi wake ukamilika utatatua changamoto ya mahitaji ya ofisi kwa watumishi wa Mahakama na wadau wake wakiwemo Mawakili wa Serikali na wa Kujitegemea, Jeshi la Polisi, Chuo cha Mafunzo, Ustawi wa Jamii, Msaada wa Kisheria, wananchi kwa ujumla na mahabusu wanao fika kusikiliza mashauri. Aidha, nimeonyeshwa namna jengo hili lilivyosanifiwa kukidhi mahitaji ya sasa na ya wakati ujao na kwamba limezingatia pia mifumo yote ya kiusalama na matumizi ya Teknologia ya Habari na Mawasiliano.


Ndugu Viongozi na wananchi wote,

Serikali inaendelea kuwekeza fedha nyingi katika ujenzi wa miundombinu ya majengo ya ofisi, hivyo ni wajibu wa watumiaji wa miundombinu hii na wananchi kwa ujumla kuitunza ili iweze kudumu kwa miaka mingi ijayo. Kudumu kwa majengo haya kunahitaji matunzo endelevu, usafi na matumizi sahihi ya umeme na mashine zilizomo ndani au mifumo ya huduma mbali mbali ndani ya majengo. Hivyo, ni muhimu uongozi wa Mahakama kuandaa mkakati maalum wa matunzo ya majengo yake yote yanayojengwa ili uimara na haiba yake vibakie kwa miaka mingi ijayo pasina kutetereka.


Ndugu viongozi na ndugu wananchi

Nihitimishe hotuba yangu kwa kukushukuru kwa dhati Mheshimiwa Jaji Mkuu, Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Zanzibar pamoja na wote walioshiriki katika maandalizi ya hafla hii inayoakisi maadhimisho ya miaka 61 ya Mapinduzi Matukufu ya mwaka 1964. Kwa dhati kabisa niishukuru na kuipongeza Serikali ya Mapinduzi Zanzibar chini ya uongozi wa Mhe. Daktari Hussein Ali Mwinyi kwa hatua zake za kuujengea uwezo Muhimili huu wa Mahakama ili uweze kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi na uhuru zaidi.


Niwashukuru pia viongozi na wananchi wote mliofika na kujumuika katika sherehe hii. Bila shaka, uwepo wenu hapa una maana kubwa katika kuyaenzi Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar ambayo tarehe 12 Januari, 2025 yatatimiza miaka 61. Kipekee nimpongeze Mshauri Mwelekezi anaesimamia ujenzi huu Kampuni ya EDGE Consult pamoja na Mkandarasi Kampuni ya Ujenzi ya JKU kwa kazi wanazoendelea kuzifanya. Niwahimize kukamilisha ujenzi huu kwa wakati na kwa ufanisi mkubwa ili jengo hili lianze kutumika kama ilivyopangwa.


Mwisho lakini si kwa umuhimu, niwashukuru na kuwapongeza wenzetu wa Muhimili huu wa Mahakama hususani Waheshimiwa Majaji na Waheshimiwa Mahakimu kwa kuendelea kutekeleza wajibu wenu wa kutafsiri sheria na kusimamia utoaji wa haki nchini. Niwaombe na kuwasihi kuendelea kutekeleza majukumu hayo kwa ufanisi, weredi na uadilifu mkubwa. Niwasihi pia wadau wote kuendelea kuuheshimu Muhimili huu na kulinda uhuru wake ili wasikutane na vikwazo wakati wa utekelezaji wa majukumu hayo muhimu. Serikali kwa upande wetu tutaendelea kujenga miundombinu wezeshi ikiwemo majengo kama haya ili kuwawezesha kufanya kazi katika mazingira mazuri kiutendaji.


Asanteni sana kwa kunisikiliza

__________


Unguja

High Court, Vuga
ZANZIBAR
Tel: +255 719 606 436
Email: info@judiciaryzanzibar.go.tz
Monday - Friday: 07:30am - 09:30pm
Saturday & Sunday: Closed

Pemba

High Court, Chake-Chake
ZANZIBAR
Tel: +255 719 606 436
Email: infopemba@judiciaryzanzibar.go.tz
Monday - Friday: 07:30am - 09:30pm
Saturday & Sunday: Closed