JAJI MKUU AWAAFISHA MAKADHI WA MIKOA
HOTUBA YA MHE. JAJI MKUU WA ZANZIBAR
KWENYE HAFLA
YA KUAPISHWA MAKADHI WAPYA WA MIKOA.
PAHALA: MAHKAMA KUU TUNGUU
TAREHE: 17/12/2024
Wahe.
Majaji wa Mahkama Kuu mliopo,
Mhe.
Mwenyekiti, Tume ya Utumishi ya Mahkama na Wajumbe wako wote,
Mhe.
Kadhi Mkuu,
Mhe.
Naibu Kadhi Mkuu,
Wahe.
Kadhi wa Rufaa mliopo,
Mhe.
Mrajis wa Mahkama Kuu
Mtendaji
Mkuu wa Mahkama,
Mhe.
Kaimu mrajis wa Mahkama ya Kadhi,
Rais wa Chama Cha Mawakili
Wahe.
Naibu Warajis wa Mahkama Kuu mliopo,
Muwakilishi
kutoka Wizara ya Nchi Afisi ya Rais,
Katiba,
Utumishi na Utawala Bora,
Muwakilishi
kutoka Afisi ya Mufti Mkuu,
Muwakilishi
kutoka Kamisheni ya Wakfu na Mali ya Amana,
Wakurugenzi
wote wa Mahkama mliopo,
Wahe.
Mahakimu na Makadhi mliopo,
Mawakili
wa Serikali na Binafsi mliopo,
Wafanyakazi
wote wa Mahkama,
Wanahabari,
Waalikwa
wote,
Mabibi
na mabwana,
ASALAMU ALAIKUM:
Kwanza
kabisa, hatuna budi kumshukuru M/Mungu mwingi wa rehma na utukufu kwa
kuturuzuku neema ya uhai na afya njema na kutuwezesha kuhudhuria hapa
kushuhudia tukio hili adhimu la kihistoria la kuapishwa kwa Waheshmiwa Makadhi
watano (5) wa Mkoa kwa Mikoa ya Unguja na Pemba baada ya kuteuliwa na Tume ya
Utumishi ya Mahkama.
Aidha,
napenda kuchukua fursa hii kuwashukuruni nyote mliohudhuria kwa kuacha majukumu
yenu muhimu na kukubali kuhudhuria kwenye shughuli yetu hii. Sambamba na hayo
na kwa kiupekee, nachukua fursa hii kuwapongeza sana Makadhi walioapishwa leo
ambao ni (1) Mhe. Omar Sheha Khamis (2) Mhe. Abdulrahman Omar Bakar (3) Mhe.
Masoud Said Abdalla (4) Mhe. Abdul – Aziz Saleh Juma na, (5) Mhe. Abdalla Hamad
Salum kwa kuteuliwa kuwa Makadhi wa Mkoa.
Kwa niaba ya Mahkama Kuu ya Zanzibar, ninawatakia kila la kheri na
mafanikio katika kutekeleza majukumu yenu mapya.
Vilevile,
natoa wito kwa wale wote ambao waliomba nafasi hizi na hawakubahatika, kwamba,
wawe wastahmilivu na waendelee kuchapa kazi huku wakielewa kuwa, hali hiyo,
haimainishi kwamba, hawana uwezo bali ni kutokana na uchache tu wa nafasi, na
kwa kweli bado zipo fursa nyingi tu zilizo mbele yao.
Wahe.
Makadhi na waalikwa wote;
Napenda
ieleweke kuwa, uteuzi huu wa Makadhi wa
Mahkama za Kadhi za Mkoa, umekuja
kufuatia uamuzi wa Serikali yetu ya Mapinduzi ya Zanzibar wa kutunga Sheria
Mpya ya Mahkama za Kadhi Nam. 8 ya 2023 ambayo pamoja na mambo mengine, imeanzisha
nafasi ya Kadhi wa Mahkama ya Kadhi ya Mkoa, kwa lengo la kutanuwa wigo zaidi katika
upatikanaji wa haki kwa mashauri ya
Mahkama za Kadhi. Kwa mnasaba huo, nachukua fursa hii kuipongeza sana
Serikali yetu na pia, naipongeza sana Tume ya Utumishi ya Mahkama kwa kusimamia
vizuri na kwa uadilifu mkubwa mchakato wote wa usaili wa waombaji walioomba nafasi hizi za Makadhi wa Mkoa hadi
hatua hii ambapo leo tunafurahia kupata Makadhi wa mikoa. Kwa kweli, nikiwa
mkuu wa mhimili huu wa Mahkama, nimeridhishwa na namna zoezi hilo
lilivyofanyika kwa haki, bila ya upendeleo wala ushawishi wa aina yoyote.
Wahe.
Makadhi na waalikwa wote;
Nitakuwa
mchoyo wa fadhila, kama sitatowa shukrani zangu binafsi kwa Waziri wa Nchi
Ofisi ya Rais Katiba, Sheria, Utumishi na Utawala Bora Mhe. Mwalimu Haroun Ali
Suleiman pamoja na Wizara yetu ya Katiba,
Sheria, Utumishi na Utawala Bora kwa ujumla, kwa mashirikiano yake makubwa kwa mhimili wetu wa Mahkama hususan kwa
kutupatia kibali cha kuajiri makadhi hawa watano (5) pamoja na watumishi mbali
mbali wa Mahkama.
Wahe.
Makadhi na waalikwa wote;
Mahkama
ya Kadhi si chombo kipya katika utaratibu wa kimahkama Zanzibar, bali ni
Mahkama kongwe ambayo awali ilianzishwa katika utawala wa Sultani katika mfumo
usiokuwa rasmi kisheria mwaka 1832, ambapo kabla ya hapo jamii ilikuwa ikitatua
migogoro yake kwa kupitia Mashekhe ndani ya jamii husika.
Katika
kipindi cha Himaya ya Muingereza mbali na kuanzishwa kwa mfumo wa Mahkama
nyengine mwaka 1897, Mahkama ya Kadhi pia iliimarishwa zaidi na kuwekewa
taratibu zake maalumu kisheria. Mahkama ya Kadhi ilipita katika vipindi tofauti
katika utendaji wake wa kazi za utoaji wa haki na usimamizi wa sheria, ambapo Mahkama
hii kabla na baada ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar ya 1964, iliongozwa na
Dikrii mbalimbali za Mahkama ikiwemo Dikrii ya mwaka 1966 ambayo ilifanya
mabadiliko madogo tu.
Mnamo
mwaka 1985, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ilianzisha rasmi Mahkama za Kadhi
chini ya Mahkama Kuu ya Zanzibar kwa Sheria Nam. 3 ya 1985, ambayo pia ilifanyiwa
marekebisho madogo na Sheria Nam. 4 ya 2003. Kuanzishwa kwa Mahkama za Kadhi kumetokana
na msingi wa kikatiba kwa mujibu wa kifungu cha 100 cha Katiba ya Zanzibar ya
1984 kinacholipa Baraza la Wawakilishi la Zanzibar mamlaka ya kuanzisha Mahkama
nyenginezo chini ya Mahkama Kuu. Vilevile tukirudi katika kifungu cha 5 cha
Sheria ya Mahkama Kuu Nam. 2 ya 1985 kimebainisha mahkama zilizochini ya
Mahkama Kuu ambapo miongoni mwazo ni Mahkama za Kadhi.
Katika
kuzipa nguvu zaidi Mahkama za Kadhi, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar mwaka
2017 ilifanya marekebisho makubwa kwa kufuta Sheria Namba 3 ya 1985 na
kupatikana sheria mpya, Sheria Namba 9 ya 2017, ambapo sheria hiyo vilevile
ilikuja kufutwa hivi karibuni na Sheria mpya ya Mahkama za Kadhi Nam. 8 ya 2023
kwa lengo la kuendana na wakati, kuongeza ufanisi pamoja na kutanua wigo katika
upatikanaji wa haki, ikiwa ni pamoja na uanzishaji wa ngazi ya Mkoa ambayo leo
hii kwa mara ya kwanza tumeanza utekelezaji wake kwa kuwateuwa Makadhi wa Mkoa,
kwani ngazi hii haikuwepo katika katika muundo wa Mahkama za Kadhi katika sheria
zote zilizotangulia kuanzisha Mahkama za Kadhi Zanzibar.
Wahe.
Makadhi na waalikwa wote;
Jukumu
la kuhukumu na kufanya haki baina ya waliohasimiana ni kubwa na zito mno. Hivyo,
kupitia hafla hii, napenda nitowe wito kwa Waheshmiwa Makadhi wa Mkoa ambao
mmekula viapo hivi punde, kuzitumikia nafasi mlizopewa kwa kutenda haki na
kufanya kazi kwa bidii, uadilifu na kwa ubunifu wa hali ya juu huku mkijuwa
kuwa, nafasi mlizozipata ni amana kutoka kwa Mwenyezi Mungu Mtukufu ambapo
atatuuliza siku ya kiama namna tulivyozitumikia nafasi zetu.
Mwenyezi
Mungu Mtukufu anatuasa katika Qur-an sura ya 4 aya ya 58 kama alivyosema; na
hapa ninanukuu tafisiri yake:
"Na
mnapohukumu baina ya watu muhukumu kwa uadilifu"
Pia tuikumbuke, bali iwe ndio dira yetu kauli
ya Mtume juu yake rehma na amani pale aliposema; na hapa ninanukuu tafsiri yake:
"Mwenye
kutawalishwa jukumu la kutoa maamuzi ya kimahkama, bila shaka amechinjwa bila
ya kutumia kisu"
Hapa
napenda ieleweke kwamba, licha ya kuwa aya na hadithi nilizonukuu zimejikita
zaidi katika kusisitiza uadilifu, lakini pia tuna wajibu wa kutambua kuwa
kufanya shughuli za kimahkama kwa uadilifu na haki kuna malipo makubwa mbele ya
Mwenyezi Mungu, hili linathibitishwa na Swahaba Abdallah Bin Masoud pale aliposema;
na hapa ninanukuu tafsiri yake:
“Wallahi, kufanya kazi ya kutoa hukumu (kwa haki)
siku moja tu, basi kwangu ni bora kuliko ibada ya miaka sabiini”
Wahe.
Makadhi na waalikwa wote;
Jukumu
kuu la Mahkama ni kutoa haki ambapo kimsingi jukumu hili ni la kiungu, hivyo tuna
wajibu wa kufahamu kwamba Mwenyezi Mungu anakuwa pamoja na Kadhi, Hakimu au
Jaji pale tu atakapotenda haki na kufanya uadilifu, ama pale anapoanza
kuikaribisha dhulma na kwenda kinyume na maadili ya kazi yake, Mwenyezi Mungu
hujitenga naye na huanza kutawaliwa na shetani.
Kwa
muktadha huo, kupitia shughuli hii, ninatowa wito kwenu makadhi wapya na
wakongwe kwamba, mfanye kazi kwa kujiamini na kufuata sheria na msikubali kuingiliwa
na mtu ama taasisi yoyote katika kutekeleza majukumu yenu. Aidha, napenda
muelewe kuwa, nyinyi ni vioo vya jamii na kwa hivyo, mnapaswa kufanya kazi zenu
kwa kuzingatia maadili ya viongozi wa umma pamoja na kujiepusha na rushwa za
aina zote.
Sambamba
na hayo, ninawakumbusha waheshmiwa Makadhi na viongozi wote wa Mahkama kuwa,
kujaza Fomu za Tamko la Viongozi wa Umma
kuhusu raslimali na madeni, ni miongoni mwa maadili na kutokujaza fomu hizo
ni kuvunja maadili. Hivyo, sote tujazeni fomu hizo kabla ya muda kumalizika
tarehe 31/12/2024.
Wahe.
Makadhi na Waalikwa wote;
Sote
tunaelewa kuwa jukumu la msingi la Mahkama ni kupokea, kusikiliza na kutolea
maamuzi mashauri yote ya jinai na madai, sambamba na kutenda haki kwa wananchi
wote bila ya chuki, woga ama upendeleo vilevile kuhakikisha kuwa maamuzi yanatolewa
kwa uweledi na haraka.
Katika
kuhakikisha hili linatendeka sambamba na kulinda maadili, Mahkama imetayarisha
Kanuni za Maadili (Code of Conduct) zinazowagusa watumishi wote wa Mahkama, pia
tumeanzisha Kamati ya Maadili ya Mahakimu, Makadhi na Watumishi wengine wa
Mahkama inayoongozwa na Jaji wa Mahkama Kuu, vilevile kuna kitengo cha
usimamizi wa maadili ambacho kinaongozwa na Naibu Mrajis wa Mahkama Kuu. Lengo
letu ni kuhakikisha kuwa watumishi wa Mahkama wanafanya kazi zao kwa misingi ya
maadili ya hali ya juu ili kuongeza na kukuza
imani ya wananchi na Serikali kwa mhimili wa Mahkama.
Wahe.
Makadhi na Waalikwa wote;
Napenda
niwaeleze kuwa, Mahkama za Kadhi zina umuhimu mkubwa kwa maisha ya wazanzibari
ambao kwa asilimia kubwa ni waislamu. Kwa sababu hiyo, asilimia kubwa ya
mashauri ya kijamii yanayowahusu waislamu kama vile ndoa, talaka, mgawanyo wa
mali iliyopatikana kwenye ndoa baina ya wanandoa, mirathi, wasia, hiba, wakfu,
matunzo na malezi ya watoto na kadhalika husikilizwa kwenye Mahkama hizi.
Kwa
kuona umuhimu huo, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar chini ya uongozi wa Mheshimiwa
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Hussein Ali Mwinyi,
imechukuwa hatua kubwa za kuandaa
mazingira mazuri ya utendaji kazi na utoaji haki kwa Mahakama za Kadhi pamoja
na Mahkama za kawaida kwa ujumla.
Miongoni
mwa hatua hizo ni ujenzi unaoendelea wa majengo ya kisasa ya Mahkama Unguja na
Pemba ambapo majengo yote hayo yana ofisi za kutosha pia kwa Mahkama zetu za
Kadhi. Vilevile kutangazwa kwa Sheria mpya ya Mahkama za Kadhi Nam. 8 ya 2023 pamoja
na kanuni za uendeshaji wa mashauri katika Mahkama hizo ni miongoni mwa mambo
yatakayoziwezesha Mahkama za Kadhi Zanzibar kufanya kazi zake kwa uweledi
mkubwa zaidi kama zilivyo mahkama za kawaida sambamba na kuzipa mamlaka pale
inapobidi, Mahkama za Kadhi kutoa adhabu kwa wale wote watakaopatikana na hatia
ya kudharau na kukaidi amri za Mahakama.
Wahe.
Makadhi na Waalikwa wote;
Katika
kipindi hichi tumeshuhudia maboresho makubwa kwa upande wa Mahkama za Kadhi na
Mahkama za kawaida kwa ujumla, ikiwa ni pamoja na ongezeko la Makadhi kwa
upande wa Mahkama zetu za Kadhi na watumishi wengine wa Mahkama, maslahi bora
kwa watumishi wote wa Mahkama, mafunzo mbali mbali ya kuwajengea uwezo makadhi
na watumishi wengine wa Mahkama sambamba na kupatiwa vifaa vya kutendea kazi
kama vile Kompyuta aina ya laptops na vishkwambi.
Vilevile
kumekuwa na ongezeko la fedha za kuendeshea ofisi (O.C) kwa shughuli za Mahkama
ya Kadhi, hivyo kutoa fursa kwa Mahkama hizi kuweza kuendesha baadhi ya mambo
yake muhimu bila ya kugongana na Mahkama Kuu, kama ambavyo kumekuwa na ushirikishwaji
mkubwa wa makadhi katika shughuli zote za kimahkama.
Kwa
kweli, hatuwa zote hizo zilizochukuliwa na Serikali na Uongozi wa Mahkama,
zimeifanya Mahkama za Kadhi kuwa ni za kisasa zaidi na zinayokwenda na wakati
na kuondokana na hali iliyokuwepo zamani ambapo Mahakama za Kadhi zilionekana
kama uchochoro mdogo ndani ya mhimili wa Mahkama na hata kupelekea baadhi ya watu
kuzidharau. Hivyo, kutokana na hatua
hizo za Serikali, hivi sasa hadhi ya Mahkama zetu za Kadhi kitaifa na kimataifa
imekuwa, na nina kila sababu ya kusema kuwa, hayo ni mafanikio makubwa kwetu
ambapo tunapaswa kujipongeza.
Wahe.
Makadhi na Waalikwa wote;
Napenda
kuchukuwa fursa hii kuwapongeza Makadhi wote kwa utendaji kazi wenu mzuri na wa
kizalendo. Kwa kweli malalamiko dhidi ya Mahkama za Kadhi yamekuwa ni machache
mno. Hukumu zinazotolewa sio tu kuwa zinakidhi viwango vya kisheria lakini pia
ni hukumu zilizofanyiwa tafiti za kina (well reserched judgments) ambapo wasomi
mbali mbali na wanafunzi wanaweza kuzitumia katika tafiti zao. Aidha, wadaawa
hupatiwa mienendo ya mashauri kwa haraka, kwa hivyo hongereni sana.
Kitu
ninachotaka kusisitiza kwa Makadhi wapya na hata wale wa zamani ni kwamba,
tusiridhike na viwango vyetu vya elimu tulivyonavyo bali tujiongeze kwa
kujifunza zaidi katika nyanja tofauti ili tusiachwe nyuma na mabadiliko ya
sayansi na teknologia yanayotokea ulimwenguni.
Kwa
mfano, hivi sasa miamala mingi inayohusu migogoro ya Mahkama za Kadhi kama vile
ndoa, talaka na mizozo mbali mbali huhusisha tehama, na kwa hivyo hatuna budi
kujifunza zaidi fani hii ya teknologia ya habari na mawasiliano ili tufanye
kazi zetu kwa ufanisi wa hali ya juu kama vile mshairi mmoja wa kiarabu
alivyosema, na hapa nanukuu tafsiri yake:
“Kuwa mwenye kupata faida kila siku kwa kuongeza
elimu na ogelea kwenye bahari ya faida”
Wahe.
Makadhi na Waalikwa wote,
Mashirikianao
na wadau (stakeholders cooperation) ni moja kati ya eneo muhimu katika utendaji
wa kazi zetu. Mahkama haitaweza kufanya kazi kwa ufanisi ikiwa peke yake, ni
lazima tukuze mashirikiano na wadau wetu mbali mbali. Kwa mnasaba huu, hivi
karibuni, kwa makusudi tumechukua hatua ya kuanzisha Kamati ya Kusukuma Mbele
Mashauri ya Mahkama za Kadhi ambayo, wajumbe wake ni maofisa kutoka Mahkama
ya Kadhi na wadau wengine mbalimbali, kama vile Chama cha Mawakili, Afisi ya
Mufti Mkuu, Kamisheni ya Wakfu na Mali ya Amana, nakadhalika.
Hivyo,
naendelea kusisitiza kufanyika kwa vikao vya kamati hiyo kwa kila robo mwaka.
Uzoefu unaonyesha kuwa, kamati hizi husaidia sana katika kusukuma usikilizaji
wa mashauri kwa haraka pamoja na kuondoa changamoto zinazojitokeza katika
utekelezaji wa shughuli zetu na kupunguza misuguano au kuonesheana vidole baina
ya Taasisi zetu za haki.
Wahe.
Makadhi na Waalikwa wote,
Kwa
kumalizia, napenda nitowe wito kwa watumishi wote wa Mahkama kubadilika na
kuacha kufanya kazi kwa mazowea bali tuhakikishe tunafanya kazi kwa kuzingatia
sheria tukiongozwa na uadilifu, uweledi pamoja na uwajibikaji wa hali ya juu.
Mwisho
kabisa, nawatakieni nyote kila la kheri na mafanikio katika kutekeleza majukumu
yenu.